Sunday 12 February 2023

RC MRINDOKO AKOSHWA NA MRADI ULIOTEKELEZWA KWA FEDHA ZA HEWA UKAA.

Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko akizungumza na Wananchi pamoja na wanafunzi baada ya kutembelea na kukagua miradi mbalimbali Halmashauri ya Tanganyika.

MKUU wa Mkoa wa Katavi Mhe.Mwanamvua Mrindoko ameridhishwa na utekelezaji wa mradi wa Ujenzi wa nyumba ya Walimu yenye uwezo wa kubeba watumishi wawili iliyojengwa kwa Fedha za hewa ukaa katika Kijiji cha Lwega Kata ya Mwese Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika.

Februari 10, 2023 katika ziara ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo Wilayani Tanganyika Mkuu wa Mkoa Mrindoko amewapongeza Viongozi wa Kata na Vijiji pamoja na kamati mbalimbali za ujenzi kwa kufanikisha Ujenzi wa Jengo hilo ambalo  hadi sasa limegharimu kiasi cha Shilingi Milioni 94.
Nyumba ya walimu (Two in One) inayojengwa katika Kijiji cha Lwega Kata ya Mwese Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika kupitia fedha za mradi wa hewa ukaa. Mradi huu umefikia hatua ya umaliziaji.

Mhe Mrindoko amehimiza Walimu kutimiza wajibu wao kikamilifu Shuleni hapo kwa kuwa Serikali imetimiza wajivu wake kikamilifu katika kujenga mazingara wezeshi kwa wao kufanya kazi shuleni hapo.

Aidha amewataka Wananchi kutosikiliza kelele kuhusu miradi inayotekelezwa kwa fedha za hewa ukaa na badala yake waelekeze jitihada zaidi katika utunzaji wa misitu kusudi waweze kunufaika zaidi na matunda ya utunzaji wa Misitu Kijijini hapo.

Miradi mingine inayotekelezwa kwa fedha zitokanazo na mapato ya hewa ukaa baadhi yake ni pamoja na Zahanati ya Lugonesi, Zahanati ya Mpembe, Vyumba vya madarasa, Nyumba za walimu Kijiji cha Lwega na jengo la utawala Shule ya Sekondari Mwese.


Picha ya 1,2 na 3 ni mradi wa ujenzi wa nyumba ya watumishi katika Zahanati ya Lugonesi iliyofikia hatua ya upigaji ripu na Zahanati ya Lugonesi ambayo imefikia asilimia 90 na miradi inajengwa kwa fedha za hewa ukaa.

Mradi wa ujenzi wa Zahanati ya Mpembe Kata ya Katuma unaotekelezwa kupitia fedha za mradi wa hewa ukaa.


Vyumba vya madarasa vilivyojengwa kwa fedha zitokanazo na fedha za mradi wa hewa ukaa.
Mradi wa ujenzi Jengo la utawala Shule ya Sekondari Mwese kupitia fedha za hewa ukaa,ujenzi wake umekamilika.
Mradi wa ujenzi Ofisi ya Kijiji Lwega, mradi umejengwa kwa fedha za hewa ukaa.

No comments:

Post a Comment