Monday 30 January 2023

TANGANYIKA YAVUKA LENGO LA KITAIFA LA KUPANDA MITI MILIONI 1.5 KILA HALMASHAURI.

Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Mhe. Onesmo Buswelu kwenye Picha ya pamoja na Wakuu wa Idara mbalimbali wa Halmashauri ya Wilaya ya Tangayika, Wanafunzi na baadhi ya Wananchi baada ya kumaliza zoezi la kupanda miche ya Miti 350 katika Makazi ya Watumishi Majalila.


HALMASHAURI ya wilaya ya Tanganyika Mkoani Katavi leo januari 30,2023 imeendelea na zoezi la upandaji miti ambapo mkuu wa wilaya ya Tanganyika Onesmo Buswelu amewaongoza Wakuu wa Idara mbalimbali na baadhi ya wananchi kupanda miti katika nyumba za Watumishi zilizopo eneo la Majalila.

Miti hiyo imepandwa pembezoni mwa Barabara ya Polisi kuelekea mtaa wa nyumba za Watumishi.

Mkuu wa wilaya Onesmo Buswelu amesema jumla ya miti 350 imependwa leo eneo hilo na kufanya jumla ya miti iliyopandwa katika halmashauri ya wilaya ya Tanganyika hadi sasa kufika Miloni 214,750 na kuifanya halmashauri hiyo kuvuka lengo la kitaifa linaloitaka kila halmashauri kupanda miti isiyopungua Milioni 1.5

"Nitoe wito kwa wasimamizi wetu wote, Viongozi wote kusimamia miti hii istawi vizuri. Tunatamani miti hii usife mti hata mmoja na isife lazima itunzwe na ilindwe"





Picha mbalimbali zikiwaonyesha wakuu wa Idara Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika katika zoezi la upandaji Miti katika Nyumba za Watumishi.

Aidha, amewaonya wenye mifugo kulisha kwenye miche iliyopandwa na mazao ya wakulima pamoja na Wananchi wanaong'oa na kuiba miche iliyopandwa kuacha tabia hiyo mara moja.

Nae Meneja TFS Wilaya ya Tanganyika Saimon Peter amesema zoezi hilo ni endelevu katika maeneo mbalimbali ya halmashauri hiyo licha ya kuwa wameshavuka lengo kwani miti bado ipo kwenye vitalu na watahakikisha inasambazwa kwenye Taasisi mbalimbali ili ipandwe.
Meneja TFS Wilaya ya Tanganyika Saimon Peter akielezea zoezi la upandaji Miti katika Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika.

Katika hatua nyingine, DC Buswelu amemtembelea mkulima wa Mahindi, Karanga, Alizeti, Pamba na Tumbaku Bw. Abdalah Kakoso na kushuhudia uwekezaji mkubwa uliofanywa na mkulima huyo, hii ikiwa ni ukaguzi wa jitihada za Serikali baada ya kutoa mbolea ya ruzuku kama imefanyiwa kazi sawa na malengo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan la kuwakwamua wakulima.

DC Buswelu amempongeza mkulima huyo na kutoa wito kwa maafisa Kilimo kuendelea kutoa ushauri kwa wakulima ili Kilimo chao kiwe na tija.





Kwa upande wake Abdalah Kakoso ameishukuru Serikali kwa kuwawezesha wakulima kupata mbolea ya ruzuku tofauti na mwanzo ilivyokuwa inauzwa kwa bei holela hali iliyowafanya washindwe kupanua kilimo chao.

"Nimshukuru sana Rais wetu Mama Samia amefanya kazi nzuri sana kwenye Kilimo kwani tulikuwa tunanunua mbolea shilingi 140,000 mfuko mmoja lakini ametoa ruzuku kwa hiyo sasahivi ni elfu sabini nafikiri kila mkulima anajitahidi kununua"

Pia ameishukuru Serikali ya Tanganyika kwa kuwa karibu na wakulima hasa kitendo cha Mkuu wa wilya kumtembelea kimpempa nguvu na kuahidi kufuata maelekezo na ushauri anaopewa.

MWISHO.

Tuesday 24 January 2023

DC JAMILA AHIMIZA UPANDAJI NA UTUNZAJI WA MITI HALMASHAURI YA WILAYA TANGANYIKA.


Mkuu wa Wilaya ya Mpanda Jamila Yusuf ambaye pia alikuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa upandaji Miti Wilaya ya Tanganyika lililofanyika Shule ya Sekondari Majalila akizindua zoezi hilo kwa kupanda mche wa Mti aina ya Mparachichi.

MKUU wa wilaya ya Mpanda Jamila Yusuf leo Januari 24,2023 amewaongoza wakazi wa halmashauri ya wilaya ya Tanganyika katika uzinduzi wa zoezi la upandaji miti katika shule ya sekondari Majalila ikiwa ni mwendelezo wa upandaji Miti milioni 2,014,000 katika Halmashauri hiyo.

DC Jamila amesema Serikali kupitia Ofisi ya Rais ikishirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira imeendelea kuratibu utekelezaji wa kampeni ya kitaifa ya upandaji na utunzaji wa miti inayotekelezwa nchini kwa kila Halmashauri kupanda miti milioni 1.5 kila mwaka.

Amesema "kila Halmashauri imewekewa malengo ya kupanda miti isiyopungua Milioni 1.5 kwa mwaka 2022/23 na kuhakikisha maeneo yote yaliyotengwa katika shughuli za uhifadhi yanahifadhiwa kikamilifu kwa mujibu wa sheria ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi yanayoukabili ulimwengu kwa sasa".




Sambamba na hayo Jamila ameagiza kuchukuliwa hatua kwa yeyote atakayekamatwa akiharibu mazingira huku akionya siasa kutoingizwa kwenye suala zima la utunzaji wa mazingira.

"Yeyote anayeleta hitilafu, uharibifu wa mazingira asiangaliwe usoni, hata kama ni Kiongozi mwenzetu awajibishwe kwa mujibu wa sheria"

Kupitia hafla hiyo, DC Jamila ametoa wito kwa Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika,Wakala wa Misitu (TFS) na Wakala wa Maji vijijini (RUWASA) kuainisha maeneo yote ya vyanzo vya maji kisha iwekwe mikakati ya kupanda miti kuzunguka vyanzo hivyo.

Awali akitoa taarifa kwa mgeni rasmi katika hafla hiyo, Afisa maliasili na utalii Wilaya ya Tanganyika, Bruno Nicolaus amesema jumla ya miche milioni 2.14 ya miche ya matunda, Kivuli na mbao ilioteshwa mwaka 2022 kwa ajili ya kupandwa katika maeneo mbalimbali ya Halmashauri hiyo.

Mkoa wa Katavi leo Januari 24,2023 umezindua zoezi la upandaji Miti litakalofanyika kila Halmashauri ambapo kilele chake kitahitimishwa Manispaa ya Mpanda tarehe 26,2023 ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko.


KAMATI YA SIASA (CCM) WILAYA YA TANGANYIKA YAWATAKA WATUMISHI KUSIMAMIA ILANI.



Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Tanganyika Yasin Kiberiti akieleza jambo baada ya kamati ya siasa kumaliza ukaguzi wa mradi wa ujenzi wa Jengo la wagonjwa wa nje (OPD) katika kituo cha Afya Ipwaga.

KAMATI ya siasa ya Chama Cha  Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Tanganyika ikiongozwa na Mwenyekiti wake Yasin Kiberiti Jana Januari 23,2023 imeanza ziara ya siku tano ya kutembelea na kukagua miradi ya maendeleo.

Wakiwa katika mradi wa ujenzi wa Jengo la wagonjwa wa nje (OPD) katika kituo cha Afya Ipwaga, Mwenyekiti Kiberiti amesema ameridhishwa na hatua ambayo miradi yote waliyotembelea imefikia huku akisisitiza usimamizi zaidi ili miradi hiyo ikamilike kwa wakati na kuwanufaisha wananchi.

Aidha, ametoa wito kwa viongozi ambao ni wasaidizi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kuendelea kusimamia Ilani ya CCM kwa kile alichodai dhamira ya chama hicho ni kuhakikisha wananchi wanafaidi matunda ya chama hicho.

"Serikali yetu iko makini na ni jukumu letu Chama Cha Mapinduzi kuisimamia Serikali na kuishauri"
Picha mbalimbali zikiwaonyesha wajumbe wa Kamati ya Siasa Wilaya ya Tanganyika na Wataalam.

Pia ameshauri halmashauri kusaidia fedha ili kuboresha ujenzi wa mradi wa Zahanati Kijiji cha Kapemba unaotekelezwa kwa fedha za mfuko wa jimbo ambao toka mwaka 2017 mradi uanze kujengwa hadi sasa mradi huo umekwama katika hatua za umaliziaji.

Kwa upande wake mwakilishi wa mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika ambaye pia ni Afisa mipango Deus Luziga amesema  Halmashauri iko tayari kuwaunga mkono wananchi katika miradi iliyoanzishwa kwa nguvu zao endapo watazingatia utaratibu wa kufikisha mradi hatua ya lenta.

Kamati hiyo jana imetembelea mradi wa ujenzi wa nyumba ya Mganga Kijiji cha Kapemba wenye thamani ya Tsh. Milioni 50 sambamba na ujenzi wa mradi wa zahanati ya Kijiji hicho, ujenzi wa mradi wa maji vijiji vya Isenga, Ifumbura na Kapemba unaoghalimu zaidi ya Tsh. Bilioni 1.3, mradi wa ujenzi wa Zahanati ya Kijiji cha Isubangala.

Miradi mingine ni ujenzi wa Zahanati ya Kijiji Mganza iliyoibuliwa kwa michango ya Wananchi na mradi wa ujenzi wa jemgo la wagonjwa wa nje (OPD) katika kituo cha afya Ipwaga.



Picha ya kwana ni Mradi wa Nyumba ya Waganga iliyojengwa kwa ajili ya Watumishi watakaohudumia katika Zahanati inayojengwa Kijiji cha Kapemba (picha ya Pili) kupitia fedha za Mfuko wa Jimbo.



Picha namba moja ni ujenzi wa mradi wa tenki la maji vijiji vya Isenga, Ifumbura na Kapemba unaoghalimu zaidi ya Tsh. Bilioni 1.3. Picha namba Mbili ni chanzo cha maji kitakachotumika katika tenki hilo.

Mradi wa ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje (OPD) katika Kituo cha Afya Ipwaga.

MWISHO.

Sunday 22 January 2023

MIGOGORO INACHELEWESHA MAENDELEO - DC BUSWELU.


Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Mhe. Onesmo Buswelu akihutubia Wananchi waliojitokeza viwanja vya Shule ya Msingi Mpanda Ndogo Kijiji cha Majalila Kata ya Tongwe wakati akizindua Wiki ya Sheria Wilayani humo.


MKUU wa wilaya ya Tanganyika Mkoani Katavi Onesmo Buswelu ametoa wito kwa wazazi na walezi kuhakikisha wanawapeleka watoto wao shule ili hapo baadae Taifa liweze kupata Mahakimu na Majaji wa kutosha.

Ametoa wito huo wakati akizindua wiki ya sheria kiwilaya leo Januari 22,2023 alipokuwa akihutubia Wananchi waliojitokeza eneo la viwanja vya Shule ya Msingi Mpanda Ndogo Kijiji cha Majalila Kata ya Tongwe.

Pia DC Buswelu ametoa wito kwa Mahakimu na watoa huduma wote katika wiki ya sheria maeneo mbalimbali wilayani humo kutumia nafasi hiyo kuwaelimisha wananchi umuhimu wa elimu na kuwakumbusha kuwa mtoto kupata elimu ni takwa la kisheria.

Aidha, amehimiza Wananchi kutumia fursa hii ya wiki ya sheria kujitokeza kueleza changamoto zinazowakabili badala ya kukaa na migogoro bila suluhu hali ambayo inaweza kupelekea kujichukulia sheria mkononi.

"Migogoro inachelewesha maendeleo, nitoe wito kwa wananchi, Mkisikia matangazo haya jitokezeni njooni mpate elimu bure hamtalipia kwa sababu Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan anatoa mishahara, anatoa uwezeshaji ili (Mahakimu) waweze kuwafikia. NJOONI MPATE ELIMU HII BURE"


Katikati ni mgeni rasmi katika uzinduzi wa Wiki ya Sheria wilaya ya Tanganyika ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Mhe. Onesmo Buswelu, Kulia ni Shaban Juma Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Tanganyika na kushoto ni Glory Mwakihaba, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya ya Tanganyika.

Kwa upande wake Glory Mwakihaba, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi amesema moja ya changamoto walizobaini ni pamoja na wananchi walio wengi kutopenda njia ya usuluhishi  kwa kuamini kuwa kazi ya mahakama ni moja tu ya kufunga watu gerezani.

Amesema kupitia wiki ya sheria watapata nafasi ya kuwaelimisha wananchi kuwa usuluhishi ni njia bora na rahisi katika utatuzi wa migogoro inayotumika duniani na kuwaondoa hofu kuwa kesi huchelewa kukamilika na kuchukua muda mrefu ni kwa sababu ya kufuata sheria na taratibu za usuluhishi ili uamuzi unapotolewa pande zote zipate haki.

Hata hivyo amesema kuwa katika Wilaya hiyo kwa muda mfupi waliofanya kazi wamebaini kuwa vitendo vya kujichukulia sheria mkononi, matukio ya ukatili wa kijinsia, mauaji zikiwemo mimba za utotoni ni matukio yanayo ongoza kujirudia mara kwa mara hivyo watajikita katika kutoa elimu zaidi kwa wananchi.


Glory Mwakihaba, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi.


Jengo la Mahakama ya Wilaya ya Tanganyika.

Kwa upande wao baadhi ya wananchi wameshukuru kwa kuogezewa huduma ya sheria karibu huku wakisisitiza changamoto walizonazo hasa vitendo vya ukatili.

"Tunashukuru kwa sisi wakazi wa hapa maana changamoto tulizonazo ni nyingi sana, ukiangalia vitendo vya kikatili vinavyotendeka ni vingi sana tulikuwa tunafikiria tutayapeleka wapi malalamiko yetu"- amesema Noriath Kakuta,mkazi wa kitongoji cha Majalila.

Kauli mbiu ya mwaka huu inasema "Umuhimu wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi katika kukuza uchumi endelevu: wajibu wa Mahakama na wadau" ambapo uzinduzi huo Kitaifa umezinduliwa Jijini Dodoma na Mgeni Rasmi akiwa ni Makamu wa Rais Dkt. Philip Mpango.

Kauli hii imebeba ujumbe muhimu kuhusu wajibu wa mahakama na wadau katika kutumia njia ya usuluhishi kutatua migogoro kwa lengo la kukuza uchumi endelevu ambapo wiki hii ya Sheria ni wakati wa Mahakama na wadau  kuwaelimisha wananchi faida za kutatua migogoro kwa njia ya usuluhishi.




MWISHO.

Saturday 21 January 2023

MKUU WA MKOA KATAVI AWATAKA WATENDAJI KUTATUA MIGOGORO YA WANANCHI KABLA HAIJAFIKA NGAZI ZA JUU.


Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko akitoa maelekezo kwa Watendaji wa Kata, Vijiji na Mitaa katika kikao kazi kilichofanyika Jana Januari 20,2023 katika Ukumbi wa Mpanda Mancipal Social Hall.



MKUU wa mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko amekerwa na baadhi ya watendaji kushindwa kutatua kero za wananchi kwa wakati hali inayowalazimu kuwatafuta Viongozi wa ngazi za juu ikiwemo Ikulu.

Kufuataia hali hiyo, Mrindoko amewataka viongozi wote mkoani humo kujiwekea utaratibu wa kusikiliza kero za wananchi na baada ya hapo apate ripoti ya hali ya migogoro na utatuzi wake kila baada ya Mwezi ili kumsaidia Rais kutatua changamoto zilizo ndani ya uwezo wao kabla hazijamfikia.

Akizungumza katika kikao kazi na Watendaji wa Kata, Vijiji na Mitaa kilichofanyika Jana Januari 20,2023 katika Ukumbi wa Mpanda Mancipal Social Hall RC Mrindoko amesema viongozi hao kushindwa kuwa karibu na wananchi kumepekelea baadhi ya kero zilizotakiwa kutatuliwa ngazi ya Mtaa, Kijiji, Kata au halmshauri kufikishwa kwa viongozi wa TAMISEMI hadi Ikulu jambo ambalo hajapendezwa nalo.

"Nisisitize, kila mmoja ahakikishe kero zinazotatulika kwenye levo yake azitatue kikamilifu na ukishazitatua umpe majibu mlalamikaji na mlalamikiwa pamoja na mamlaka nyingine zinazohusika kwa sababu zitaturahisishia kwamba mgogoro flani umeshatatuliwa kwa njia hii na sasa tutalitazama utatuzi wake kama bado unalalamikiwa ulikuwa halali au sio halali na tutaona hatua nzuri za kuchukua ili kumaliza jambo hilo "




Aidha, amewataka viongozi hao kuwa waadilifu kwa kutenda haki pale mwananchi anapofikisha lalamiko lake, kujiepusha na vitendo vya rushwa ili wananchi wawe na imani na uongozi wao hasa kunapotolewa suluhu la jambo flani.

"Niwatake kuhakikisha msiwe chanzo cha kuzalisha kero mpya, msiwe chanzo cha kuzusha migogoro kati ya watumiaji wa Ardhi na hasa kwenye eneo hili kuna baadhi ya Viongozi wasio waaminifu wanatuvuruga,badala ya kufanya uongozi wa kutatua matatizo, kero na changamoto wanakuwa ni mwanao wa kuzalisha migogoro"

RC Mrindoko amesema Serikali haitamvumilia kiongozi yeyote atakayekuwa chanzo cha kuzalisha migogoro mipya hasa kiongozi kushiriki kupima maeneo ambayo fika anajua ni yawazi au eneo moja kuuzwa zaidi ya mara mbili huku yeye akiwa shuhuda kiongozi huyo atachukuliwa hatua za kisheria.

Amewataka kabla ya kufanya uamuzi wowote, wajiridhishe kwanza na eneo husika kwa kuwasiliana na uongozi wa juu.

"Wananchi wetu wanatupa taarifa, kama wewe Mtendaji hauko vizuri hata kama hawatasema mbele yako tuko kwenye mkutano tukiondoka watatutumia meseji, watatupigia simu jamani anayevuruga mambo yote ni Mtendaji wa mtaa, anayetuvurigia mambo yote hapa ni Mtendaji wetu wa kijiji. Naomba mkasimame kwa uadilifu unaostahili katika utumishi wa Umma"

Pia amewataka kuwa karibu na wananchi ili iwe vyepesi kwao kufikisha kero kwa wakati kabla hajachukua uamuzi wa kuwatafuta Viongozi wa ngazi za juu.

MWISHO.