Friday 17 February 2023

WATUMISHI NA WATENDAJI TANGANYIKA WATAKIWA KUZINGATIA MAADILI.

Katibu Tawala Wilaya ya Tanganyika Geofrey Mwashitete.

WATENDAJI na watumishi wa Wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi wametakiwa kutimiza wajibu na kuzingatia maadili ya kazi kipindi wanapokuwa wanatekeleza majukumu yao.

Wito huo umetolewa na Katibu Tawala Wilaya ya Tanganyika Geofrey Mwashitete katika kikao kazi cha kutoa mafunzo kwa watumishi, kilichoongozwa na Katibu huyo kilichofanyika eneo la shule ya Msingi Bulamata Kata ya Bulamata Tarafa ya Kabungu hapo jana Februari 16, 2023.

Mwashitete amesema lengo la mafunzo hayo ni kuwapitisha watumishi kwenye kanuni, taratibu na sheria mbalimbali za utumishi wa umma ili waweze kutimiza wajibu wao.

"Tumepokea maagizo kutoka kwa waziri mkuu pamoja na Mh. Rais Samia Suluhu Hassan aliagiza siku nyingi kwamba tunatakiwa siku 2 tuwepo ofisini lakini siku 3 twende tukasimamie miradi mbalimbali pamoja na kutembelea wadau pamoja na wananchi wanaohitaji huduma mbalimbali"amesema

Ameongeza kuwa mafunzo hayo yamelenga kuwakumbusha watumishi wa umma kwamba muda mwingi wautumie kuwahudumia wananchi pamoja na wadau mbalimbali na viongozi wanaohusika kuhudumia wananchi kama maafisa ugani na afisa mifugo wafike kwa wananchi badala ya kusubiri kufuatwa maofisini.

Kwa upande wake Kaimu afisa utumishi Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika, Andrew Chiduo amesema kuwa lengo la kuwafuata watendaji na watumishi katika Tarafa hiyo ni kuwakumbusha haki na wajibu wao katika majukumu yao huku wakitarajia ufanisi zaidi katika kazi.

Kaimu afisa utumishi Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika, Andrew Chiduo.

Nao baadhi ya watumishi mara baada ya kupata mafunzo hayo wameahidi kuleta mabadiliko chanya katika majukumu yao kama watumishi wa umma.

"Tumekumbushwa mambo mengi ambayo mengine tuliyasahau, tumekumbushwa kudai haki zetu za msingi baada afisa utumishi kutukumbusha haki na wajibu ambao inatakiwa tupate na tufanye ili tupate haki zetu" amesema Justin Erasto,Afisa Mtendaji Kata ya Bulamata.



MWISHO.

Thursday 16 February 2023

RC KATAVI AAGIZA KUCHUKULIWA HATUA KALI WAZAZI AMBAO HAWAJAWAPELEKA WATOTO KUANZA MASOMO.

Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Mridoko akizungumza na Wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Mwese.

MKUU wa Mkoa wa Katavi Mhe.Mwanamvua Hoza Mridoko ameagiza kuchukuliwa hatua kali za kisheria kwa wazazi ambao bado hawajawapeleka watoto kuripoti kidato cha kwanza.

Mkuu wa Mkoa Mrindoko ametoa agizo hilo katika ziara yake 10 Februari 2023 katika Shule ya Sekondari ya Mwese alipotembelea shuleni hapo kwa lengo la kukagua maendeleo ya Ujenzi wa Jengo la Utawala lililojengwa kwa fedha zitokanazo na mradi wa Hewa ukaa.

“Nimeambiwa hapa Wanafunzi walioripoti ni 149 bado wanafunzi 15 hawajaripoti,muda uliotolewa na Serikali umekwisha pita,Nimtake Mhe. DC wa Wilaya hii ya Tanganyika hawa watoto watafutwe na wazazi wao wachukuliwe hatua,tunahitaji kujenga kizazi chenye maarifa na manufaa katika Taifa hili”,alisema Mkuu wa Mkoa Mrindoko.




Aidha Mhe.Mrindoko ametoa rai kwa  Wanafunzi Shuleni hapo kuunga mkono jitihada za Serikali  na kumtendea haki Mhe.Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kusoma kwa bidii  kwa kuwa Serikali imetimiza kikamilifu wajibu wake wa kujenga mazingira wezeshi kwa Wanafunzi na Walimu  Nchini.

Amewataka Wanafunzi hao kutunza miundombinu ya Majengo pamoja na samani kusudi miundombinu hiyo iweze kudumu kwa muda mrefu zaidi.

Katika hatua nyingne Mkuu wa Mkoa Mrindoko ameupongeza uongozi wa Shule ya Sekondari ya Mweze,Kamati za Ujenzi pamoja na Uongozi wa Kata ya Mwese kwa kusimamia ubora  na viwango katika ujenzi wa Jengo la Utawala Shuleni hapo.

Awali katika Taarifa yake Mkuu wa Shue ya Sekondari ya Mwese ameeleza kuwa mradi wa ujenzi huo ulianza utekelezaji wake Desemba 2021 ambapo hadi kukamilika kwake mradi  utagharimu kiasi cha shilingi Milioni Mia Moja arobaini ambapo hadi sasa Shilingi  Milioni mia moja thelathini na nane na laki nane  zimekwisha tumika  huku ujenzi ukiwa katika hatua za mwisho kabisa  za umaliziaji.

Katika hatua nyingine Wananchi wa Kijiji cha Kapanga Wilayani Tanganyika Mkoani Katavi wameeleza kushangazwa na kufurahishwa na utitiri wa miradi mbalimbali ya maendeleo ndani ya muda mfupi inayotekelezwa Kijijini hapo.

Wananchi wameeleza hayo mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe.Mwanamvua Hoza Mrindoko alipotembelea Kijiji hicho kwa lengo la kukagua mradi wa maji pamoja na Ujenzi wa Zahanati inayojengwa kupitia Fedha za Mradi wa Hewa Ukaa. Wananchi hao wameipongeza Serkkali ya awamu ya Sita chini ya Mhe.Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo miradi mbalimbali ya maendeleo imekuwa ikitekelezwa Kjijijini hapo. Pamoja na Pongezi Wananchi hao walimueleza Mkuu wa Mkoa wa Katavi kuwa kwa sasa changamoto kubwa kijijini hapo ni upatikanaji wa Mtandao wa uhakika ambapo kwa muda mrefu Mawasiliano ya simu yamekua changamoto.
“Tunampongeza sana Mhe.Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa miradi mingi ambayo inaendelea,changamoto yangu kubwa kwa sasa ni upatikanaji wa Mtandao na tumekuwa tukipata shida sana na hasa walimu ambao wamepatiwa vishkwambi wamekuwa wakipata changamoto ya mtandao,unawakuta wamerundikana sehemu moja wakitafuta mtandao. Hii ni shida ikipatiwa ufumbuzi mambo mengine yatakwenda” Alisema Zefania Sleni Mkazi wa Kijiji cha Kapanga.

Kufuatia changamoto hiyo Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe.Mwanamvua Mrindoko aliwatoa hofu Wananchi wa Kijiji hicho ambapo amewaeleza kuwa atalifikisha suala hilo kwa Waziri Mwenye dhamana ya Mawasiliano pamoja na kufanya ufuatiliaji wa karibu kusudi kupata ufumbuzi wa changamoto hiyo. Amewaeleza Wananchi wa Kapanga kuwa maendeleo yanayofanyika kijijini hapo ni jitihada za Serikali ya Dkt Samia Suluhu Hassan na kwamba hizo ni rasharasha tu mambo mazuri zaidi yanakuja.
Aidha amewataka Wananchi kuendelea kuunga mkono jitihada za Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kutoa ushirikiano wa uhakika ikiwa ni pamoja na kulinda miundombinu ya Maji ili Wananchi waweze kunufaika zaidi na miradi hiyo.

MWISHO.

Sunday 12 February 2023

RC MRINDOKO AKOSHWA NA MRADI ULIOTEKELEZWA KWA FEDHA ZA HEWA UKAA.

Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko akizungumza na Wananchi pamoja na wanafunzi baada ya kutembelea na kukagua miradi mbalimbali Halmashauri ya Tanganyika.

MKUU wa Mkoa wa Katavi Mhe.Mwanamvua Mrindoko ameridhishwa na utekelezaji wa mradi wa Ujenzi wa nyumba ya Walimu yenye uwezo wa kubeba watumishi wawili iliyojengwa kwa Fedha za hewa ukaa katika Kijiji cha Lwega Kata ya Mwese Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika.

Februari 10, 2023 katika ziara ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo Wilayani Tanganyika Mkuu wa Mkoa Mrindoko amewapongeza Viongozi wa Kata na Vijiji pamoja na kamati mbalimbali za ujenzi kwa kufanikisha Ujenzi wa Jengo hilo ambalo  hadi sasa limegharimu kiasi cha Shilingi Milioni 94.
Nyumba ya walimu (Two in One) inayojengwa katika Kijiji cha Lwega Kata ya Mwese Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika kupitia fedha za mradi wa hewa ukaa. Mradi huu umefikia hatua ya umaliziaji.

Mhe Mrindoko amehimiza Walimu kutimiza wajibu wao kikamilifu Shuleni hapo kwa kuwa Serikali imetimiza wajivu wake kikamilifu katika kujenga mazingara wezeshi kwa wao kufanya kazi shuleni hapo.

Aidha amewataka Wananchi kutosikiliza kelele kuhusu miradi inayotekelezwa kwa fedha za hewa ukaa na badala yake waelekeze jitihada zaidi katika utunzaji wa misitu kusudi waweze kunufaika zaidi na matunda ya utunzaji wa Misitu Kijijini hapo.

Miradi mingine inayotekelezwa kwa fedha zitokanazo na mapato ya hewa ukaa baadhi yake ni pamoja na Zahanati ya Lugonesi, Zahanati ya Mpembe, Vyumba vya madarasa, Nyumba za walimu Kijiji cha Lwega na jengo la utawala Shule ya Sekondari Mwese.


Picha ya 1,2 na 3 ni mradi wa ujenzi wa nyumba ya watumishi katika Zahanati ya Lugonesi iliyofikia hatua ya upigaji ripu na Zahanati ya Lugonesi ambayo imefikia asilimia 90 na miradi inajengwa kwa fedha za hewa ukaa.

Mradi wa ujenzi wa Zahanati ya Mpembe Kata ya Katuma unaotekelezwa kupitia fedha za mradi wa hewa ukaa.


Vyumba vya madarasa vilivyojengwa kwa fedha zitokanazo na fedha za mradi wa hewa ukaa.
Mradi wa ujenzi Jengo la utawala Shule ya Sekondari Mwese kupitia fedha za hewa ukaa,ujenzi wake umekamilika.
Mradi wa ujenzi Ofisi ya Kijiji Lwega, mradi umejengwa kwa fedha za hewa ukaa.

Saturday 11 February 2023

CCM TANGANYIKA YAAHIDI USHIRIKIANO KUFIKIA MALENGO YA KUKUSANYA BILIONI 40.3

MWENYEKITI wa chama cha mapinduzi (CCM) wilaya ya Tanganyika mkoa wa Katavi Yasin Kiberiti amesema hana wasiwasi na halmashauri ya Tanganyika kufikia na hata kuzidi lengo la kukusanya na kutumia Tsh. Bilioni 40.3 endapo vyanzo vya mapato vitasimamiwa vizuri.

Ameyasema hayo katika kikao cha baraza maalumu la madiwani la kupitia na kujadili rasimu ya bajeti ya mwaka 2023/24, kikao kilichofanyika Jana Februari 10, 2023 katika ukumbi wa mikutano wa Mkurugenzi.

"Na sisi tutakutana na wenzetu Ofisi ya Mkuu wa wilaya kwa maana ya kusimamia bajeti kuhakikisha mapato yote tuliyojiwekea, mamilioni haya tuliyojiwekea yanakamilika lakini yanazidi hizo asilimia. Tukisimamia vizuri naamini hizo zitazidi"

Mwenyekiti wa chama cha mapinduzi (CCM) wilaya ya Tanganyika mkoa wa Katavi Yasin Kiberiti.

Naye Katibu Tawala wilaya ya Tanganyika Geofrey Mwashitete amesema ili kufikia malengo hayo wataandaa mazingira mazuri kwa mamlaka za Serikali za mitaa ikiwemo kutoa ushirikiano.

"Kwa kweli inaonekana ni bajeti nzuri na kubwa kwa sababu kama mwaka huu mapato ya ndani imepangwa Bilioni 10 na milioni 12 ikilinganishwa na mwaka jana tulikuwa kwenye Bilioni tano na kidogo kwa hiyo tumepaa na tafsili yake ni kwamba mambo mengi yatatekelezwa"

Katibu Tawala wilaya ya Tanganyika Geofrey Mwashitete.

Akihitimisha kikao hicho Mwenyekiti wa halmashauri ya Tanganyika Hamad Mapengo amewashukuru madiwani kwa michango yao pamoja kuipitisha rasimu ya bajeti ya mwaka 2023/24 iliyowasilishwa na Afisa mipango wilaya ya Tanganyika Deus Luziga.

Aidha, amesema mapendekezo yote yaliyopendekezwa ikiwemo kuongeza vyanzo vya mapato vitazingatiwa kwa kuwa vitaiongezea halmashauri mapato jambo litakalowezesha kutekeleza miradi mbalimbali hadi ya ziada.

Mwenyekiti wa halmashauri ya Tanganyika Hamad Mapengo.




Sehemu ya wajumbe waliohudhuria kikao hicho.

MWISHO.

Wednesday 8 February 2023

HALMASHAURI YA TANGANYIKA KUKUSANYA TSH. BILIONI 40.3 MWAKA WA FEDHA 2023/24.

PICHA: Kushoto ni Mwenyekiti wa Kikao cha kamati ya ushauri Wilaya (DCC) Wilaya ya Tanganyika ambaye pia ni mkuu wa wilaya Onesmo Buswelu akiteta jambo na Mkurugenzi mtendaji Juma Shabani (mwenye miwani) pamoja na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Tanganyika Hamad Mapengo.

HALMASHAURI ya wilaya ya Tanganyika mkoa wa Katavi katika bajeti ya mwaka wa fedha 2023/24 inatarajia kukusanya na kutumia kiasi cha Tsh. Bilioni 40.3, ikiwa ni ongezeko la asilimia 23.5 ya bajeti ya mwaka 2022/23 ya Tsh. Bilioni 32.6

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Tanganyika Juma Shaban leo Februari 8, 2023 alipokuwa akiwasilisha taarifa ya rasimu ya bajeti mbele ya wajumbe katika Kikao cha kamati ya ushauri Wilaya (DCC) Wilaya ya Tanganyika kilichoongozwa na mwenyekiti wake ambaye pia ni mkuu wa wilaya ya Tanganyika Onesmo Buswelu kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Mkurugenzi.

Mkurugenzi huyo amesema chanzo cha bajeti hiyo kuongezeka ni kutokana na kuongezeka kwa makisio ya mishahara ya Watumishi, vyanzo vya mapato hasa chanzo cha mrahaba unaotokana na hewa ukaa, uuzaji wa Viwanja, kuongezeka kwa mazao ya kilimo na kutokana na kukua kwa biashara ya mazao ndani na nje ya Nchi.

Amesema Halmashauri hiyo imepanga kukusanya kiasi hicho cha fedha kutoka katika vyanzo mbalimbali vya mapato ikiwemo mapato ya ndani, fedha za ruzuku kutoka Serikali kuu na ruzuku kutoka kwa wafadhili na wahisani.

"Kwanza tuna mapato ya ndani ambayo yana jumla ya Bilioni 10 ambayo bajeti hii imeongezeka ukilinganisha na bajeti ya mwaka uliopita, kutokana na kuongezeka kwa bajeti matumizi mengineyo ni asilimia 40 na miradi ya maendeleo itakuwa asilimia 60"

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Tanganyika Juma Shaban akiwasilisha mpango wa rasimu ya bajeti kwa Mwaka wa fedha 2023/24 katika kikao cha DCC kilichofanyika leo katika Ukumbi wa mikutano wa Mkurugenzi.

Aidha ameongeza kuwa "kuna chanzo ambacho ni fedha za hewa ukaa ambazo hizi ni mapato fungiwa kwa sababu fedha hizi zinaenda moja kwa moja kwenye Vijiji husika ambapo imekadiriwa kupokea Bilioni Nne na Milioni mia mbili na kumi na mbili elfu"

Amesema bajeti hiyo imezingatia kukamilisha ujenzi wa miradi ya maendeleo iliyoanzishwa kwa nguvu za wananchi ikiwemo kuimarisha sekta ya afya, elimu na Maliasili.

Mikakati mingine ni kujenga shule ya mchepuo wa kingereza (English medium) ili kutatua tatizo la aina hiyo ya shule katika Halmashauri, kuboresha kituo cha Afya Sibwesa kuwa cha mfano, kuboresha Hospitali ya Ikola na kuanzisha kituo cha nyuki cha kuchataka asali sambamba na kukarabati nyumba zipatazo 14 za Halmashauri zilizopo Mpanda mjini ukiwemo ukumbi wa Idara ya Maji.

Katika sekata ya Maji akiwasilisha rasimu ya bajeti Mhandisi wa Wakala wa Usambazaji wa Majisafi na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) wilaya ya Tanganyika Festo Mpogole amesema katika mwaka wa fedha 2023/24 RUWASA wilayani Tanganyika imepanga kutumia Tsh. Bilioni 1.6 kutekeleza miradi mbalimbali ya maji.

Nae mwakilishi kutoka Wakala wa Barabara za mijini na vijijini (TARURA) wilaya ya Tanganyika Mhandisi Bonventure Katambi amesema jumla ya Tsh. Bilioni 4.7 zinatarajiwa kutumika katika matengenezo ya barabara wilayani humo.


PICHA ya kwanza ni Mhandisi wa Wakala wa Usambazaji wa Majisafi na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) wilaya ya Tanganyika Festo Mpogole na Picha ya pili ni Mhandisi Bonventure Katambi kutoka Wakala wa Barabara za mijini na vijijini (TARURA) wilaya ya Tanganyika wakiwasilisha taarifa.

Akihitimisha Kikao hicho, Mwenyekiti wa kikao ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika, Onesmo Buswelu amehimiza kupanga mipango mathubuti ya ukusanyaji mapato ili kufikia adhima ya utekelezaji wa miradi.

Aidha, ametumia kikao hicho kutoa wito kwa Watumishi kutimiza wajibu wao kwa kuchapa kazi na kuzingatia ufanisi huku akiwaomba Viongozi wa Dini kuwaombea Viongozi ili waweze kutimiza majukumu yao ya kuwatumikia wananchi.

Mwenyekiti wa Kikao cha kamati ya ushauri Wilaya (DCC) Wilaya ya Tanganyika  ambaye pia ni mkuu wa wilaya Onesmo Buswelu akitoa maelekezo wakati akifunga kikao.

Rasmu hiyo ya bajeti inatarajiwa kusomwa na kupitishwa katika kikao cha bajeti cha baraza la madiwani siku ya Ijumaa tarehe 10 Februari 2023.










Picha mbalimbali zikiwaonyesha wajumbe waliohudhuria kikao Kikao cha kamati ya ushauri Wilaya (DCC) Wilaya ya Tanganyika

MWISHO.

Sunday 5 February 2023

RC KATAVI ATAJA MAFANIKIO YA MKOA KATIKA MAADHIMISHO YA MIAKA 46 YA CCM.

MKUU wa mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko amesema kwa kipindi cha Miaka miwili na nusu chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan mkoa na taasisi zake umetumia zaidi ya Tsh. Bilioni 620 katika kutekeleza miradi mbalimbali.

Mhe. Mrindoko amesema katika sekta ya elimu mkoa umepata vyumba vya madarasa 119 katika shule za sekondari na kuwezesha wanafunzi 14,854 waliofaulu kidato cha kwanza kuweza kupata Sehemu ya kusomea.

Amesema sekta ya afya mkoa wa Katavi umepata Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ambayo imeanza kutoa huduma, Hospitali 5 za wilaya, vituo vya Afya zaidi ya 14 na Zahanati zaidi ya 20 ambapo miradi hiyo yote imetekelezwa kwa fedha za mapato ya ndani, Serikali kuu na zingine kutoka kwa wafadhili na wadau mbalimbali.

Mhe. Mrindoko ametaja mafanikio mengine ya chama cha mapinduzi katika sekta ya maji kuwa mkoa wa Katavi umefikia asilimia 70.7 ya upatikanaji wa maji vijijini na asilimia 60 mjini huku Mpanda mjini ikitarajia kufikisha asilimia 100 ya upatikanaji wa maji kupitia mradi wa "miji 28" unaotarajia kutekelezwa katika mwaka huu wa fedha.

Kadhalika RC Mrindoko amesema katika sekta ya miundombinu yapo mafanikio makubwa ikiwemo mkoa kuunganishwa na mikoa mbalimbali kwa kiwango cha lami na kiasi cha Tsh. Bilioni 4 kinatarajiwa kutumika kukarabati barabara za miji na vijijini kupitia TARURA ikiwemo ujenzi wa madaraja makubwa likiwemo daraja la Mto Msadya na daraja la Ifinsi.

"Mheshimiwa mwenyekiti kama ulivyotuagiza barabara hii ya inayoingia eneo la Kabatini ni barabara ambayo ina hali mbaya, nikuhakikishie barabara hii imetengewa Milioni 200 katika mwaka wa fedha unaoanza mwezi Julai 2023 barabara hii itaweza kufanyiwa matengenezo"


Mafanikio mengine ni kutatua migogoro mbalimbali ikiwemo migogoro 74 ambayo ipo kwenye timu ya Mawaziri nane imeweza kuwasilishwa na migogoro hiyo ipo katika hatua za mwisho za utatuzi.

Aidha, aametoa wito kwa wananchi kutunza Misitu.


Baadhi ya Wananchi waliojitokeza katika mkutano wa kuadhimisha Miaka 46 ya CCM katika viwanja vya Shule ya Msingi Kabatini leo Februari 5,2023.

MWISHO.

UJUMBE WA CCM MKOA WA KATAVI KATIKA MAADHIMISHO YA MIAKA 46.

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Katavi Comred Idd Kimanta,mgeni rasmi katika maadhimisho ya Miaka 46 ya CCM.

Mwenyekiti wa Chama cha mapinduzi (CCM) Mkoa wa Katavi Comrade Idd Kimanta amewataka viongozi na wanachama wa chama hicho mkoani Katavi kuacha majungu badala yake watengeneze mahusiano mazuri na Watumishi kwa kuwa wao ndio watekelezaji wa Ilani.

Kimanta ametoa kauli hiyo leo akiwa Kijiji cha Mpembe kitongoji cha Kabatini halmashauri ya wilaya ya Tanganyika akihutubia Wananchi wa kitongoji hicho katika kelele cha maadhimisho ya miaka 46 ya kuzaliwa chama hicho.

Amesema kamati ya siasa mkoani humo haitasita kumchukulia hatua Kiongozi wa chama ambaye atabainika kuvuruga mahusiano baina ya Serikali na chama hali kadhalika kwa Mtumishi atakayebainika kuvuruga mahusiano baina ya chama na Serikali.

"Sisi wote ni Binadamu kukitokea kutoelewana basi kutoelewana huko kuzungumzwe kwa kuheshimiana, hatutarajii tufike mahali tukute Kiongozi wa chama au Kiongozi wa Serikali anamdharau mwenzake"

Amesema pamoja na kuisimamia Serikali lazima chama hicho kiilinde kwa kuiunga mkono huku akimtaka Mkuu wa mkoa huo kuwachukulia hatua Watumishi wote wazembe wanaokwamisha maendeleo ya Mkoa na ilani ya chama.

"Kwenye tenga samaki mmoja akioza toa yule aliyeoza halafu wale wengine waendelee wawe kitoweo. Mtumishi mmoja asiharibu sifa ya Watumishi wengine, toa yule wengine wazuri tunaendelea kuwa nao hakuna cha samaki mmoja akioza wote wameoza"

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Katavi Comred Idd Kimanta akitoa maelekezo kwa Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko.

Aidha, ametoa wito kwa wana CCM kutambua wajibu wao na kufanya ziara kusikiliza kero za wananchi na kuzitatua huku akiwasihii Watanzania kuendelea kuwa na imani na chama cha mapinduzi kwa kuwa ndicho chama pekee kinachoweza kutatua kero zao.

"Chama kinapokwenda ndani ya wananchi kinasikia nini wananchi wanataka. Chama lazima kila siku kisikie wananchi wanataka nini kwa sababu chama ndio kimbilio la wananchi"

Pamoja na yote, chama cha (CCM) Mkoa wa Katavi kimehitimisha maadhimisho hayo kwa kuwakabidhi kadi za uanachama wanachama wapya 2700.

Chama cha Mapinduzi (CCM) leo Februari 5,2023 kinaadhimisha Miaka 46 toka kuanzishwa kwake Februari 5, 1977.

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Katavi Comred Idd Kimanta akikabidhi kadi kwa mmoja wa wanachama wapya.