Wednesday 16 August 2023

WILAYA YA TANGANYIKA IKO TAYARI KUUPOKEA MWENGE WA UHURU AGOSTI 24,2023.

Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Mhe. Onesmo Buswelu akizungumza na Wanahabari Ofisini kwake.

Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Mhe. Onesmo Buswelu amesema Serikali wilayani humo na Wananchi kwa ujumla wamejiandaa na wapo tayari kuupokea Mwenge wa Uhuru utakao wasili wilayani humo Agosti 24 mwaka huu na kupokelewa eneo la Kijiji cha Vikonge ukitokea mkoani Kigoma kabla ya kukabidhiwa Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda Agosti 25,2023.

DC Buswelu ameyasema hayo Jana Agosti 15, 2023 wakati akizungumza na Wanahabari Ofisini kwake eneo la Mpanda ndogo, Ifukutwa.

Amesema Mwenge wa Uhuru baada ya kupokelewa utafanya mkesha Kasekese kabla ya kukimbizwa kukagua, kuzindua na kuweka mawe ya msingi katika miradi mbalimbali.

Aidha, Mhe. Buswelu ameitaja miradi itakayotembelewa na Mwenge wa Uhuru kuwa ni pamoja na uzinduzi wa mradi wa maji uliopo Kijiji cha Vikonge uliogharimu kiasi cha zaidi ya Tsh. milioni Mia sita na nane, pia Mwenge utatembelea Klabu za Lishe, Klabu za kupinga na kupambana na rushwa sambamba na kutembelea miradi upandaji miti pamoja na kutembelea kikundi cha Vijana ambao wananufaika na mkopo wa Halmashauri.

Mhe. Buswelu ameongeza kuwa, miradi mingine ni pamoja na kutembelea na kuzindua jengo la wagonjwa wa nje (OPD) katika Kituo cha Afya Sibwesa, kuzindua Shule mpya ya msingi Kasekese, kutembelea na kukagua barabara inayounganisha Kagunga na Kasekese iliyokarabatiwa kwa kiasi cha Tsh. milioni 300.

"Eneo lingine ambalo Mwenge wa Uhuru utatembelea ni kwenye ujenzi wa Zahanati ya Kagunga. Mradi huu ni mradi ambao umetekelezwa kwa fedha ambazo zinatokana na mapato ya hewa ukaa ambayo inatokana na utunzaji wa mazingira"- Aliongeza DC Buswelu.

Kadhalika, Mkuu huyo wa Wilaya amesema baada ya kutembelea mradi wa Zahanati hiyo litafuata zoezi la upandaji miti katika viunga vya Zahanati hiyo ikiwa ni ishara ya Wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mapambano ya kulinda na kutunza maliasili.

Hata hivyo, amesema miradi yote ambayo itatembelewa na Mbio za Mwenge wa Uhuru inagharimu kiasi cha takribani bilioni 1.9

Kauli mbiu ya Mwenge wa Uhuru mwaka huu inasema "Tunza Mzingira, Okoa vyanzo vya maji kwa Ustawi wa Viumbe hai kwa Uchumi wa Taifa"

Baadhi ya Viongozi waliohudhuria kikao cha DC na Wanahabari.

Friday 26 May 2023

DC BUSWELU AHIMIZA UKWELI KWENYE MAENDELEO AMBAYO SERIKALI INAYAFANYA

MKUU wa wilaya ya Tanganyika Mhe. Onesmo Buswelu

Mkuu wa kituo cha Polisi wilaya ya Tanganyika, ACP Kiberiti

MKUU wa wilaya ya Tanganyika Mhe. Onesmo Buswelu ametoa wito kwa watanzania kuwa wakweli katika maendeleo ambayo Serikali inayafanya pasipo kupotosha.

DC Buswelu ametoa wito huo baada ya kutembelea na kukagua hatua ya ujenzi wa kituo cha Polisi Tanganyika, ambapo amsema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuboresha mazingira ya Askari Polisi wilayani humo ikiwemo kuwajengea nyumba Watumishi wa Jeshi hilo.

Hayo yamejiri baada ya kauli ya Katibu wa chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Salumu Mwalimu akiwa ziarani wilayani humo kutoa kauli ambayo siyo ya kweli kuwa OCD hana nyumba ya kuishi wakati viongozi wengine wamejengewa nyumba na Serikali.

"kuna nyumba kubwa imeshakamilika three in one. Polisi hawajasahaulika na kazi inaendelea vizuri wapo ambao tayari wameshahamia kwenye nyumba zile, nyumba zina maji na umeme"

Nyumba ya watumishi wa Jeshi la Polisi (Three in One)

Aidha, DC Buswelu amesema licha ya kukamilisha ujenzi wa nyumba hizo, Serikali inajenga kituo cha kisasa cha Polisi kitakacho ghalimu shilingi milioni 500 ambapo ujenzi wake umefikia hatua ya kumwaga jamvi.

Kwa upande wake Mkuu wa kituo cha Polisi wilaya ya Tanganyika, ACP Kiberiti amesema kwa kiasi kikubwa uwepo wa nyumba hizo umesaidia wananchi kupata huduma ya kiusalama haraka.

ACP Kiberiti ameongeza kuwa, ujenzi wa kituo cha  Polisi ulisimama kutokana na mvua zilizokuwa zikinyesha kutokana na jeografia ya wilaya hiyo hivyo ujenzi utaendelea hivi karibuni.

MWISHO.

Monday 15 May 2023

DC TANGANYIKA AWATAKA WAZAZI KUTENGA MUDA WA KUZUNGUMZA NA WATOTO WAO.



MKUU wa Wilaya ya Tanganyika Mhe. Onesmo Buswelu ametoa wito kwa wazazi kurudi enzi za nyuma kwa kutenga muda wa kuzungumza na watoto wao mara kwa mara badala ya kuwawekea katuni kwenye runinga huku watoto wakiendelea kuharibika kimaadili.

DC Buswelu ametoa wito huo leo Mei 15,2023 katika maadhimisho ya Siku ya Familia duniani yaliyofanyika Kiwilaya katika viwanja vya Shule ya Msingi Ifukutwa, Halmashauri ya Tanganyika Mkoani Katavi.

Amesema yapo mambo yanafanywa na jamii yasiyompendeza Mungu kama mapenzi ya jinsia moja na vikiwemo vitendo vya ukatili, ukichunguza vinatokana na kukosekana kwa maadili  hivyo ipo haja ya wazazi na walezi kuwatengenezea misingi mizuri watoto wao kabla hawajaharibika.

Akilejea maneno ya Mungu katika Biblia, DC Buswelu amesema Mungu alipoona matendo maovu yamekithiri katika uso wa dunia, alichukia na kushusha gharika na sodoma na gomola ikateketea na watu wote, na ameitaka jamii kuachana na matendo maovu kabla Mungu hajachukia na kushusha gharika.

"Ili haya yatuepuke lazima turejee kwenye kuwekeza kwenye Utu, tuwekeze kwenye Ubinaadamu, tuwekeze kwenye Upendo, tuwekeze kwenye Umoja, tuyajenge maadili ya Taifa letu kuanzia ngazi ya Familia"

Mzee maarufu, Hassan Mapengo mkazi wa Tanganyika amesema zamani wazazi walikuwa na utamaduni wa kukutana na watoto wao ndiyo maana hapakuwa na matendo ya unyang'anyi, kuporomoka kwa maadili tofauti na sasa ambapo wazazi hawana muda wa kuzungumza na watoto zaidi wanarudi usiku.

MWISHO.

Monday 8 May 2023

WILAYA YA TANGANYIKA: YAWAKARIBISHA WAWEKEZAJI KWA AJILI YA KILIMO NA MIFUGO.





HAYO yamesemwa na Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika, Mheshimiwa Onesmo Buswelu alipoitembelea kampuni ya Meru Agro Wilayani Mbozi akiwa pamoja na kamati ya ulinzi ya Wilaya, Waheshimiwa Madiwani na Wakuu wa Idara.

Ziara hiyo ilifanyika Tarehe 05/05/2023 hadi Tarehe 7 ikiwa ni kuitembelea kampuni ya Meru Agro kuona namna inavyozalisha mbegu Mbalimbali, viuatilifu na vifaa vya shambani.

Mheshimiwa Buswelu alisema "Nawaomba Muje muwekeza Tanganyika, ardhi ipo ya kutosha, usalama upo na wataalam wa kufanya nao kazi wapo". Pia alisisitiza kufanya tafiti za udongo katika eneo la Wilaya hiyo ili kujua ni mbegu zipi zinafaa kutumika katika eneo hilo.

Kwa upande wake Christopher Shimwela, Meneja wa kampuni ya Meru Agro kanda ya Mbeya, alisema msimu uliopita walizalisha mbegu tani elfu tano na zote ziliisha. "Na Msimu huu tunategemea kuzalisha tani zaidi ya elfu sita"

Pia Mkurugenzi wa Meru Agro Ndugu Matanga Chacha alisema "Tupo tayari kuwekeza Tanganyika na tumeagiza mitambo ya thamani ya Shilingi Billioni 2 itakayotumika katika kilimo Wilayani Tanganyika" pia aliomba apewe ekari elfu tano kwa ajili ya uwekezaji huo.

Shabani Juma Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika alimuhakikishia muwekezaji huyo kutoa eneo la ekari elfu tano kama atafuata vigezo vilivyowekwa na Wilaya hiyo pamoja na kamati ya uwekezaji.

Pia msafara wa Mkuu wa Wilaya na Madiwani pamoja na wakuu wa Idara ulipata nafasi ya kutembelea Shamba la Mahindi lenye ekari elfu tatu lililopandwa mahindi aina ya Meru HB 515, Meru HB 513, Meru HB 405 na Meru HB 623 pamoja na mbegu za mahindi ya asili aina ya Situka M1.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri, Ahmed Mapengo alimtaka muwekezaji huyo kuwa na nia ya dhati kuwekeza katika eneo hilo. "kumekuwa na watu wengi wababaishaji na hawana nia ya kufanya uwekezaji, wanapewa maeneo na wanayatelekeza" Alisema

Wilaya ya Tanganyika imetenga eneo la Luhafwe lenye Hekta 46 elfu kwa ajili ya uwekezaji wa miundombinu ya Kilimo na Mifugo.

MWISHO.

Friday 28 April 2023

TANGANYIKA MUUNGANO CUP YATAMATIKA KWA MAJALILA FC KUIBUKA MSHINDI.

Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Mhe. Onesmo Buswelu akimkabidhi kikombe kepteni wa Majalila FC Naseeb Kakoso baada ya kuishinda bao mbili kwa sifuri timu ya Sijonga FC.

MKUU wa Wilaya ya Tanganyika Onesmo Buswelu leo Aprili 27,2023 amehitimisha mashindano ya Muungano CUP yaliyokuwa yanalindima wilayani humo kwa kukabidhi zawadi mbalimbali kwa washindi.

Timu ya Majalila FC imeibuka mshindi wa kwanza wa mashindano hayo, katika fainali iliyochezwa katika Uwanja wa michezo Majalila shule ya msingi kwa kuitandika Sijonga FC bao mbili kwa bila.

Akihutubia wakazi wa mji wa Majalila mara baada ya kumalizika kwa fainali kati ya Majalila FC dhidi ya Sijonga FC, DC Buswelu amewapongeza washiriki wote wa mashindano hayo, kwani ni njia moja wapo ya kudumisha mshikamano kama ilivyo asisiwa na waasisi wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar Hayati Baba wa Taifa Mwl. Julius Nyerere na Hayati Abeid Karume.

DC Buswelu amesema kutokana na jitihada za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika michezo, Serikali wilayani Tanganyika imekusudia katika bajeti yake ya Mwaka wa fedha huu kutenga fedha kwa ajili ya kujenga Uwanja wa kisasa wa mpira.

Kwa upande wake Kaimu mkuu kitengo cha michezo Halmashauri ya Tanganyika, Otuman Kasamya amesema katika mashindano hayo mshindi wa kwanza ambaye ni Majalila FC amepata zawadi ya shilingi elfu Themanini na kikombe, mshindi wa Pili shilingi elfu Hamsini, mshindi wa Tatu shilingi elfu 30 huku mshindi wa Insha akijipatia zawadi ya shilingi elfu Ishirini ambaye ni mwanafunzi kutoka Kakoso Sekondari na mwamuzi bora aliyejioatia shilingi elfu Ishirini.

MWISHO.

MKUU WA WILAYA YA TANGANYIKA AWEKA JIWE LA MSINGI KITUO CHA AFYA BULAMATA.



Muonekano wa Jengo la OPD Kituo cha Afya Bulamata.

MKUU wa wilaya ya Tanganyika Onesmo Buswelu Aprili 25,2023 alitembelea na kukagua mradi wa kituo cha Afya Bulamata kisha kuweka jiwe la msingi.

Kituo cha Afya Bulamata awali kilipokea shilingi milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la nje (OPD), maabara na kichomea taka kabla ya kuongezewa tena shilingi milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la kufulia, jengo la upasuaji na jengo la Mama na mtoto pamoja na ujenzi wa njia.

Mradi ulianza kujengwa mwezi Desemba 2021 na hadi sasa umekamilika na umeenza kutoa huduma kwa wananchi wa Kata hiyo na maeneo jirani.

Aidha, mara baada ya kuweka jiwe la msingi mkuu wa wilaya ya Tanganyika Onesmo Buswelu alizindua zoezi la ugawaji vyandarua bure kwa mama wajawazito waliofika kupata huduma katika kituo hicho.

"Leo tunawapa vyandarua tunaomba mkavitumie kujikinga na Malaria. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan hataki kuona mwananchi wake anapoteza maisha kwa sababu ya Malaria ndiyo maana ameleta vyandarua na Madaktari"

Mkuu wa wilaya ya Tanganyika Mhe. Onesmo Buswelu (kulia) akifuarahi na Diwani wa Kata ya Bulamata baada ya kuweka Jiwe la Msingi kituo cha Afya Bulamata.

Mkuu wa wilaya akimkabidhi chandarua mama mjamzito kama sehemu ya Serikali kuwakinga Wananchi wake dhidi ya Malaria.

Awali Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Tanganyika, Dkt. Alex Mrema alimweleza Mkuu wa Wilaya kuwa Serikali imeleta vifaa kwa ajili ya mama wajawazito ikiwemo vyandarua ambavyo vitakawiwa bure.

Baadhi ya wananchi waliofika kupata huduma katika kituo hicho wamemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwajengea kituo cha Afya karibu kwani mwanzo walikuwa napata shida kufuata huduma maeneo ya mbali.

MWISHO.

WANANCHI TANGANYIKA WAADHIMISHA MUUNGANO KWA KUIISHUKURU SERIKALI.

Msafara wa viongozi mbalimbali wakiongozwa na mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Mhe. Onesmo Buswelu ukiwa eneo la mradi wa daraja linalojengwa katika mradi wa ujenzi barabara ya Vikonge - Luhafwe (km 25). Aprili 25,2023

WANANCHI wa Halmashauri ya wilaya ya Tanganyika mkoa wa Katavi wameadhimisha Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa kuishukuru Serikali kwa kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya kutoka Vikonge hadi Uvinza mkoani Kigoma kwa kiwango cha lami.

Wakizungumza mbele ya msafara wa mkuu wa wilaya ya Tanganyika, Onesmo Buswelu aliyeambatana na viongozi wengine walipotembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa mradi wa barabara ya Vikonge - Luhafwe (km 25) Aprili 25,2023 walisema kabla ya Uhuru walilazimika kukatiza maporini kufuata huduma za Afya jambo lililosababisha vifo kwa Mama wajawazito.

"Tulipata shida sana, unakuta mama mjamzito anatoka mbali wanapopatwa na uchungu mtu anazalia njiani, kiti (mtoto) kinakataa kutoka mtu anafariki" Alisema Devotha Titto mkazi wa Kijiji cha Vikonge.

Alisema mbali na kuwarahisishia usafiri lakini pia anaimani hata kiwango cha nauli kitakuwa chini ikiwemo ufupi wa safari kutoka Mpanda hadi Kigoma kwani kwa sasa wanatumia hadi masaa Sita kufika mkoani Kigoma.

Diwani wa Kata ya Tongwe Frank Kidigasi alisema kukamilika kwa barabara hiyo ya Mpanda - Kigoma itafungua fursa kwa wakazi wa Tanganyika na Katavi kwa ujumla kufanya biashara Kigoma na nchi jirani za Congo, Rwanda na Burundi kwa kuuza mazao yao kwa kuwa mkoa wa Katavi ni wa Kilimo.

Diwani wa Kata ya Tongwe Frank Kidigasi

Awali akiwasilisha taarifa ya utekelezaji mradi huo, Kaimu Meneja Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS) mkoa wa Katavi Mhanfisi Emily Zengo alisema barabara hiyo inajengwa kwa fedha za ndani kwa ghalama ya Tsh. bilioni 35.638.

Alisema, kazi inayofanyika ni ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami, kukata sehemu ambazo milima iko juu sana, ujenzi wa daraja kubwa Mnyamasi lenye urefu wa mita 61.8 na kina cha mita 5 ambalo litakuwa suluhisho eneo hilo kwa kuwa mvua zinaponyesha maji yanapita juu ya barabara.

Kaimu Meneja Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS) mkoa wa Katavi Mhanfisi Emily Zengo.

Akizungumza baada ya kukagua mradi huo, Mkuu wa wilaya ya Tanganyika Onesmo Buswelu alisema ziara hiyo ni kuadhimisha miaka 59 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambapo amemhakikishia Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa Serikali ya Tanganyika itasimamia miradi yote kwa ufanisi ili Wananchi waweze kupata thamani ya fedha zinazotolewa na Serikali.

Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Mhe. Onesmo Buswelu akifurahia na Wananchi baada ya kutembelea mradi wa barabara katika maadhimisho ya sherehe za miaka 59 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

MWISHO.

Thursday 6 April 2023

TANGANYIKA: KISHINDO CHA SERIKALI YA AWAMU YA SITA NDANI YA MIAKA MIWILI YA UONGOZI WA RAIS DKT. SAMIA SULUHU HASSAN.


Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Mhe. Onesmo Buswelu akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM katika kikao cha Halmashauri kuu ya CCM Wilaya ya Tanganyika kwa kipindi cha miaka Miwili ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

ZAIDI ya shilingi Bilioni 131 zimekusanywa, kupokelewa na kutumika katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo iliyopo katika Wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi.

Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Onesmo Buswelu wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2020-25 katika Wilaya hiyo kwa kipindi cha miaka miwili( Machi 2021- 2023 ) cha serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Ameyasema hayo katika kikao cha Halmashauri kuu ya CCM Wilaya ya Tanganyika kilichoketi Jana Aprili 5, 2023 katika ukumbi wa Mkurugenzi Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika mkoani humo.

DC Buswelu amesema fedha hizo shilingi 131,791,925,200.5 zimefanikisha kuifungua Tanganyika katika maeneo mbalimbali ikiwemo Afya,  barabara, kilimo, elimu, maji, mawasiliano na uchukuzi, umeme vijijini, uwekezaji sanjari na sekta mbalimbali.

Katika sekta ya Afya ndani ya miaka miwili, wilaya hiyo ilipokea zaidi ya bilioni 4 ambazo zimetumika katika ujenzi wa miundombinu ya Afya kama ujenzi wa jengo la wagonjwa mahututi na ujenzi wa wodi tatu katika hospitali ya wilaya ya Tanganyika ikiwemo ujenzi wa vituo vya Afya, Zahanati na vyumba za watumishi.

Amesema, katika sekta ya barabara Wilaya ya Tanganyika sasa imeunganishwa na mtandao wa barabara hali inayochochea uwekezaji ikiwemo wananchi kujiingizia kipato kupitia usafiri na usafirishaji.

"Ujenzi wa barabara ya Vikonge - Luhafye yenye urefu wa KM 25 inayojengwa kwa fedha za kitanzania zaidi ya bilioni 35 mkandarasi yupo eneo la mradi na ujenzi unaendelea, barabara ya Kagwira - Ikola - Karema yenye urefu wa KM 120 ipo hatua ya awali ya upembuzi ambayo imefikia asilimia 95 na kiasi cha shilingi bilioni 1.073 kimetolewa" Alisema Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika, Mhe. Onesmo Buswelu

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Tanganyika Yasin Kiberiti akifuatilia taarifa ya utekelezaji wa Ilani ikisomwa na Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika




Baadhi ya Wajumbe wakifuatilia hotu ikisomwa kuhusu hatua ambayo Wilaya ya Tanganyika imepiga ndani ya kipindi cha miaka Miwili ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Samia Suluhu Hassan

Barabara nyingine zinazotengenezwa chini ya TANROAD ni ya Kibo - Mwese - Lugonesi, Kagwira - Karema na Mpanda - Uvinza huku Wakala wa mjini na vijijini TARURA akiongezewa bajeti kutoka 641,150,000 mwaka wa fedha 2020/21 hadi kufikia 4,157,455,928.18 kwa mwaka wa fedha 2022/23 sawa na ongezeko la asilimia 259.

Aidha, amesema sekta ya elimu imeimarika mara dufu baada ya kujengwa miundombinu ya kutosha  ambapo kupitia fedha za UVIKO-19 jumla ya vyumba vya madarasa 196 vimejengwa ( shule ya msingi  vyumba 127 na shule za Sekondari vyumba 69) na kupitia fedha za mapato ya ndani na hewa ukaa jumla ya vyumba 94 vimejengwa ikiwemo kujenga shule mpya ya Majalila, mabweni n.k

Pia chuo cha ufundi stadi (VETA) ujenzi wake unatarajia kuanza mwezi huu eneo la Kijiji cha Majalila.

Maeneo mengine aliyoyata wilaya hiyo kupiga hatua ni sekta ya maji ambapo shilingi 6,481,086,307.46 zimetolewa kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya maji ambapo miradi 15 itakayonufaisha vijiji 22 inajengwa na baadhi imeanza kutoa huduma.

Hata hivyo, amesema sekta ya maliasili na utalii imezidi kuimarika ambapo kutokana na utunzaji na usimamizi mzuri wa maliasili na misitu, jumla ya vijiji 8 vya Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika vimenufaika na mradi wa hewa ukaa ambapo shilingi bilioni 6.57 zimepatikana ndani ya miaka miwili.

Fedha hizo zimetumika kujenga madarasa, zahanati, kuajiri walimu wa mikataba, kutoa vyakula kwa wanafunzi shuleni, kuajiri Askari walinzi wa misitu na kukopesha vikundi vya wajasiriamali vijijini kupitia COCOBA.

Wilaya ya Tanganyika ilianzishwa mwaka 2016 ikijulikana wilaya ya Mpanda Vijijini ambapo jina la Tanganyika lilitokana na Ziwa Tanganyika lililopo kwenye mpaka wa mashariki ya eneo hili.

Katika sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022, idadi ya wakazi wa wilaya ni 371836.

MWISHO.

Tuesday 28 March 2023

TANGANYIKA: VIONGOZI WA KATA NA VIJIJI WAPEWA SEMINA YA USIMAMIZI WA MIRADI YA HEWA UKAA.

Baadhi ya Watendaji wakifatilia mafunzo ya kuwajengea uwezo katika utekelezaji na usimamizi wa miradi ya Hewa Ukaa yanayofanyika katika Ukumbi wa Mkurugenzi jengo la Halmashauri Machi 27,2023


VIONGOZI wa kata na vijiji vinavyonufaika na mradi wa hewa ukaa katika Halmashauri ya wilaya ya Tanganyika mkoa wa Katavi leo wameanza mafunzo ya siku tatu yatakayohusisha mada mbalimbali ikiwemo dhana ya utawala bora na utunzaji wa nyaraka.

Akizungumzia yatakayojadiliwa katika mafunzo hayo Mratibu wa miradi ya hewa ukaa Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika, Alfonce Mwakyusa amesema mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo watendaji wa kata na vijiji pamoja na Wenyeviti wa vijiji ili kuimarisha usimamizi utakaozingatia utawala bora, namna ya kuibua miradi hiyo na matumizi sahihi ya fedha zitokanazo na mauzo ya hewa ukaa.

Ameongeza kuwa, fedha zinazotokelewa ni nyingi ambapo katika awamu hii ya Sita na Saba vijiji nane vinavyo nufaika na mradi wa hewa ukaa vimeingiziwa Tsh. Bilioni 4.27 hivyo kutakuwa na mada kuhusu uhandisi ujenzi na mada kuhusu masuala ya rushwa.

Bw. Alfonce Mwakyusa Mratibu wa miradi ya hewa ukaa Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika.

Akifungua mafunzo hayo yanayofanyika katika Ukumbi wa Mkurugenzi Mtendaji, Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Onesmo Buswelu ambaye alikuwa mgeni rasmi, amewataka washiriki kuwa kutilia maanani mafunzo hayo kwani serikali haitataka kusikia Kijiji chochote kikienda kinyume au kuharibu mradi ikwemo udanganyifu katika kupata wazabuni.

"Yaani Vijiji vyoye 55 vifeli kuna Wilaya hapo? Wewe kwenye eneo lako unapotengeneza mikakati ya kufelisha maana yake unataka nchi yote ifeli. Unapotengeneza mikakati ya kuiba hata senti moja maana yake unataka nchi yote ifeli halafu mwisho wa siku tukimbile wapi? Mimi nawasihii, msifanye hivyo" 

Kataika hatua nyingine, DC Buswelu ameagiza kufikia Aprili mosi mwaka huu Vijiji vyote vunavyo nufaika na mradi viwe vimeingiziwa fedha kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa miradi.

Mhe. Onesmo Buswelu,Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika na mgeni rasmi katika mafunzo hayo akifafanua jambo.

Kwa upande wao washiriki wa mafunzo hayo wamesema wanaamini kupitia mada zinazowasilishwa wataenda kusimamia ipasavyo fedha na utunzaji sahihi wa nyaraka, usimamizi mzuri wa miradi kwani awali walikuwa hawana weledi na masuala hayo.



MWISHO.

Thursday 23 March 2023

SERIKALI YATENGA BILIONI 9 KUANZISHA KILIMO CHA UMWAGILIAJI KATIKA MASHAMBA YA MPUNGA YA GEREZA LA KALILANKULUKULU TANGANYIKA.


SERIKALI ya Tanzania imetenga kiasi cha Tsh. bilioni 9 kwa ajili ya kuanzisha Kilimo cha umwagiliaji katika mashamba ya mpunga ya Gereza la Kalilankulukulu katika Halmashauri ya wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi.

Akizungumza baada ya kutembelea wakulima mbalimbali Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Onesmo Buswelu amesema hadi kufikia mwezi Aprili mwaka huu kiasi cha Tsh. Milioni mia nane kitakuwa kimeshaingizwa kwa ajili ya kuanza ujenzi wa tenki la kuhifadhia maji katika eneo hilo lenye ukubwa wa takribani Ekari mia tano.

DC Buswelu amemhakikishia Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa watahakikisha wanasimamia kikamilifu na kwa ukaribu mradi huo kwa kuwa si tu utawanufaisha Magereza bali utanufaisha pia wananchi wa mkoa wa Katavi na Taifa kwa ujumla.
Onesmo Buswelu Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika.

Kwa upande wake Mkuu wa Gereza hilo, SP Bosco Paulo Lupala amesema katika msimu huu wa Kilimo wamelima Ekari 150 za zao la mpunga kwa kutumia nguvu kazi ya wafungwa ambapo wanatarajia kuvuna gunia 1700 mpaka 2000 sawa na Tani mbili za mpunga.

SP Lupala amemshukuru Rais kwa kutenga fedha kwa ajili ya kuliendeleza eneo hilo kwani ujio wa mradi huo utawapunguzia changamoto mbalimbali huku wakitarajia uzalishaji kuwa mkubwa zaidi kutokana na zana za kisasa zitakazotumika ukilinganisha na ukubwa wa eneo.
SP Bosco Paulo Lupala, Mkuu wa Gereza hilo la Kalilankulukulu.

Nae Afisa Kilimo Wilaya ya Tanganyika Philemon Mwita amesema wanaendelea kutoa elimu kwa wakulima ili watumie kanuni bora za Kilimo ikiwemo matumizi sahihi ya pembejeo.

Kufuatia mradi huo mkubwa, baadhi ya wananchi wawanaozunguka eneo hilo wamemshukuru Rais Dkt. Samia kwa kuwakumbuka na wanaamini ni mradi utakaowanufaisha ikiwemo kukabiliana na changamoto ya mvua.

Machi 22,2023 Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika akiwa ameambatana na Afisa Kilimo wametembelea wakulima wa mazao mbalimbali ikiwa ni kujionea hali ilivyo baada ya mbolea ya ruzuku iliyotelewa na Serikali kama ilitumika ipasavyo na wamejirisha uzalishaji utakuwa mkubwa kutokana na wakulima kuitumia fursa ya pembejeo ya ruzuku.